Monday, May 28, 2012

MTOTO UMLEAVYO NDIVYO AKUAVYO!


KUMJENGEA MTOTO HESHIMA BINAFSI  "Self-esteem"

Heshima binafsi (Self-esteem) ni ngao ya mwanao dhidi ya changamoto nyingi za dunia hii. Watoto wengi wanaojivunia uwepo wao ndani ya familia au mahali fulani mara nyingi wamekuwa na uwezo wa kutatua migogoro na kuzuia misukumo hasi kirahisi.
Watoto wa aina hii kila mara huwa wanatabasamu na kufarahia maisha. Watoto hawa huwa wapo wazi hawaoni aibu na wanaari ya mafanikio muda wote.
Kwa upande mwingine, watoto wasio au wenye heshima binafsi dhaifu, wanaweza kuchukulia changamoto wanazopambana nazo kama chanzo cha wasiwasi na mara nyingi hukata tamaa. Wale wenye fikra mbovu kuhusu wao wenyewe huwa wanapata wakati mgumu sana kutatua matatizo mbalimbali.
Ukimpa suala la kufikiria sana akupe jibu mfano “mimi mbaya” au “siwezi kufanya lolote vyema” atakaa kimya, ataondoka au atafadhaika tu kimya kimya. Akikutana na changamoto yoyote jibu lake la haraka ni “siwezi mimi”.
Jinsi ya kumwezesha mwanao kujijengea heshima-binafsi.

Heshima binafsi na kujiamiani ni nini?
Heshima binafsi ni mkusanyiko wa imani au hisia tulizo nazo kuhusu sisi wenyewe, yaani tunavyojitambua.
“Tunavyojielezea wenyewe mbele ya wenzetu tunashawishi vichocheo binafsi ndani yetu, fikira na tabia na tunagusa jinsi tunavyoweza kurekebisha au kuikabili mihemko yetu.
Utaratibu wa kumjengea mtoto heshima binasfi na kujitambua huanzia utotoni. Mfano, mtoto anayefikia lengo fulani kama kuwa wa kwanza darasani anajijengea ujasiri unaoimarisha heshima binafsi. Mtoto anapobadili maamuzi na kutafuta njia nyingine ya kutekeleza nia yake baada ya kujaribu na kushindwa kufanya kitu fulani mara kadhaa kunamjengea fikira za “ninaweza”.
Dhana ya mafanikio ya mtu kulingana na msimamo wake huanzia utotoni. Jinsi mtoto anavyojaribu na kushindwa, anajaribu tena na kushindwa tena na hatimaye kufanikiwa anajijengea uwezo binafsi wa kujiamini. Wakati huo huo, mtoto huyu anajijengea ufahamu binafsi na ujasiri wa jinsi ya kujichanganya na watu wengine.
Ndio maana kuhusishwa  kwa mzazi katika makuzi na malezi ya mtoto ndio njia pakee na sashihi ya kuwasadia watoto kujijengea ufahamu binafsi. Heshima binafsi pia inamaanisha hisia za kuweza, kulikochanganyika na hisia za kupendwa. Mtoto anayefurahia mafanikio fulani lakini wazazi wake hawaonyeshi kufurahia mafanikio hayo, mtoto huyo atapungukiwa na heshima binafisi na kujiamini.
Vilevile, mtoto anayehisi kupendwa lakini anaona aibu kuhusu uwezo wake pia anaweza kupungukiwa heshima binafsi. Heshima binafsi huja pale tu kunapokuwa na usawa kwenye haya mawili, yaani kutoona aibu kwa kujiamini na kuhisi anapendwa.

Dalili za heshima bora na heshima dhaifu kwa mtoto

Heshima binafsi inabadilika kulingana na mtoto anavyokua. Hubadilika na kuboreshwa mara kwa mara kwa sababu huchangiwa na uzoefu wa mtoto na ufahamu mpya anaoupata. Hivyo inamsaidia kuzitambua dalili za heshima bora na heshima dhaifu.
Watoto wanaopungukiwa heshima binafsi hawapendi kujaribu mambo mapya na mara nyingi hujishusha kuhusu uwezo wao wenyewe. “mimi mbumbumbu”, “Siwezi kujifunza namna ya kufanya hili” au “hakuna anayenijali”. Hawawezi kuhimili vipingamizi, hushindwa mapema na mara nyingi hutegea mwingine afanye.
Watoto wenye heshima binafsi na wanaojiamini hupenda kujichanganya na wengine. Hufurahia jamii inayowazunguka na shughuli zinazoendelea ndani ya jamii, mara nyingi huwa ni wadadisi wa mambo. Inapotokea changamoto, hujitahidi kupata ufumbuzi na huonyesha kutoridhika na mafanikio wanayoyapata bila ya kudharau wengine. Mfano, badala ya kusema ‘mimi zuzu’ mtoto mwenye heshima binafsi ya kujiamini atasema ‘hili silielewi’ wanajua mapungufu na uwezo wao na wanakubali hali walio nayo.

Wazazi wanawezaje kusaidia

Je, mzazi anawezaje kumsaidia mwanae kujijengea heshima binafsi na kujiamini? Vigezo vifuatavyo vinaweza kusaidia:-

1. Chunga unachoongea

Watoto wako makini sana na maneno wanayoongea wazazi wao. Kumbuka kusifia mwanao si kwa kazi nzuri tu aliyoifanya lakini pia kwa jitihada anazoonyesha katika kufanikisha jukumu fulani. Lakini inampasa mzazi kuwa mkweli. Mfano, kama mwanao amefeli darasani labda ameshika namba 28 kati ya watoto 30, unaweza kumsifia tu kama mwanzoni alikuwa wa 30. Lakini kuwa mkweli kwamba matokeo yako bado ni mabaya sana.

2. Kuwa mfano bora

Kama wewe mzazi unatabia za ukali, matusi, umekata tamaa na huonyeshi matumaini (kukosa rajua), au si mkweli kuhusu uwezo wako kama mzazi, mwanao anaweza kuakisi tabia zako.
Onyesha heshima na nidhamu kama mzazi na mtoto atajifunza kutoka kwako.
Watoto huwa wanaamini baadhi ya mambo ambayo si mazuri katika makuzi yao. Ni jukumu la mzazi kuzitambua imani potofu alizonazo mwanae na kutafuta jinsi ya kumwanisha ukweli. Mtoto anaweza kuamini kuwa mtoto ananunuliwa na hazaliwi, jaribu kutafuta mbinu za kumwaminisha ukweli kadiri anavyokua.
Mfano, mtoto anayefanya vizuri darasani lakini anashindwa kwenye somo la Hisabati, anaweza kusema ‘siwezi kufanya hesabu’ mimi sio mwanafunzi mzuri. Imani ya mtoto kujumuisha kushindwa hesabu darasani na kutokuwa mwanafunzi mzuri darasani ni imani potofu. Ukimwacha mtoto akue na imani hiyo inaweza kupelekea kushindwa baadae hata kwenye maisha yake.
Mpe moyo mwanao, mwambie ‘wewe ni mwanafunzi bora’ unafanya vizuri shuleni, Hesabu ni somo moja tu, jifunze tu sana Hesabu utailewa.

3. Onyesha wazi unampenda mwanao

Upendo unaouonyesha kwa mwanao utasaidia kumjenga kwenye kujiamini na kuimarisha heshima binafsi. Wakumbatie wanao na waonyeshe kuwa unawafurahia.
Tafuta urafiki wa karibu na mwanao. Kuwa karibu nae kwa kadiri iwezekanavyo hata kama unabanwa na kazi lakini weka mipaka pia kwenye mapenzi unayoyaonyesha kwa wanao. Watoto ni wepesi sana kutambua kama mzazi anampenda kweli au hampendi.
Ni vyema umwambie alivyo fahari yako. Andika ujumbe kuelezea unavyomchukulia na uweke mahali atakapouona ghafla akiwa mwenyewe kama vile kwenye mfuko/begi lake la shule, kitandani kwake na kwingineko. Atafurahi kila anapoona ujumbe huo.

4. Jenga mazingira safi ya malezi

Mtoto asiyejisikia salama au yule anayejiona kuwa ananyanyaswa nyumbani anaweza kujihisi yu duni. Mtoto anayelelewa na wazazi wanaogombana mara kwa mara, hukata tamaa na mwenendo wa maisha.
Watoto wa aina hii hupoteza hamu ya kuwa nyumbani kiasi kwamba hujiona wenye balaa kuzaliwa na nyie wazazi. Anaweza kujenga chuki zisizotawalika na akawa mgomvi na mbishi dalili za kujifikiria-dhaifu. Jaribu kuchunguza ikiwa mwanao ameudhiwa huko alikokuwa, kama vile shuleni ama na marafiki zake, mwulize maswali yatakayokupa picha ikiwa yeye ndiye tatizo yeye ndio chanzo cha ugonvi. Halafu mpe ushauri nasaha kwa zingatio hilo.

5. Msaidie mwanao ajifunze kujaribu

Ni jukumu la mzazi kujishughulisha sana katika kumsaidia mtoto wake awe na tabia ya kujaribu mambo. Shughuli zinazosisitiza ushirikiano wake na wenzake ni nzuri zaidi ya zile zilizokaa kimashindano zaidi. Kwa hiyo kama una watoto zaidi ya mmoja, ni vyema ukawapangia majukumu yanayofanya washirikiane. Kwa mfano, unaweza kumshauri aliye mkubwa asaidie kumfundisha mdogo wake kusoma ama kufanya hesabu. Ukiwapa kazi zenye mwelekeo wa kimashindano unaharibu. Yule ashindaye atajenga kiburi, majigambo na dharau na yule ashindwaye atajiona hawezi hasa kama zoezi hili limejirudia mara kadhaa.

6. Tafuta msaada wa wataalam

Ukiona mwanao anajengeka na kukua kwa kutojiamini, amua kutafuta ushauri wa wataalam. Wapo washauri nasaha wenye uwezo wa kumtambua mwanao na kukushauri ni kwanini anashindwa kujiamini au kujijengea heshima binafsi kwenye jamii inayomzunguka.
Hivyo, sisi wazazi tunanafasi kubwa na muhimu sana ya kuwafanya watoto wetu kujenga uwezo wa kujiamini na kuwa na heshima binafsi kuhusu maisha yao mwenyewe. Na wazazi tusipokuwa makini kwa matendo yetu jinsi tunavyowalea watoto wetu, tunawajengea udhaifu wa kujiamini hata watakapokuwa wakubwa mbele za watu.

SAIKOLOJIA NA TABIA

Maisha ya kifamilia yanapitia mambo mengi. Ni jukumu letu sisi wazazi kumtayarisha  mtoto ili aweze kukabiliana nayo. Mambo hayo yanaweza kuwa wazazi kuachana, kifo cha mzazi mmojawapo au wote, kuzaliwa kwa mtoto mwingine, tabia ya nyumbani kukiwa na wageni na kadhalika. Mtoto anastahili matayarisho ya kisaikolojia kuhusu mambo hayo. Pia jua tabia mbalimbali za mtoto kwa jinsi anavyokua hadi kufikia ujana.

Kumfunza mwanao nidhamu

Utafanyaje kumuepusha mwanao asiangalie video kwa muda mrefu kama ameshazoea? Je, mwanao akiwa shuleni kama mwanafunzi mwenzake akianzisha fujo mfano amempiga ngumi, afanyeje? na ufanyeje ili mwanao aheshimu mamlaka yako kama mzazi? Haya ni baadhi tu ya  masuala ya msingi ambayo wazazi wengi tumeshindwa kuelewa madhara yake katika kujenge nidhamu ya mtoto.
Ni vyema mzazi uwe na msimamo ambao uko wazi kwa mwanao. Ukiongelea masuala  ya mzaha iwe ni mzaha kweli, linapokuja suala la nidhamu uonyeshe unamaanisha nidhamu kweli. Kama maamuzi unayofanya yanakinzana kila mara hata mwanao ni vigumu kuyafuata.
Katika sehemu hii tunaeleza jinsi unavyoweza kuweka nidhamu ya watoto wako ndani ya familia. Nidhamu unayotakiwa kuijenga hutofautiana kati ya mtoto na mtoto kulingana na umri.

Mwaka 0 hadi miaka 2

Watoto wa umri huu mara nyingi hutaka kushika kila kitu, kumbuka ni umri huu ambapo mtoto anatambaa, anaanza kutembea, anaanza kuongea na anaanza kula vyakula mbalimbali ni vyema kuweke mbali vitu vinavyowapeleka kwenye majaribu ya kutaka kufanya jambo fulani mfano kuwasha TV, redio, kugusa vitu vya thamani, kula vitu anavyookota, dawa nk. Vitu hivi ni muhimu viwekwe sehemu ambayo watoto hawawezi kufikia.
Mzoeshe mwanao anayetambaa kumkataza, mwambie “ACHA” au “HAPANA” anapotaka kushika vitu hatari au vitu ambavyo unawasiwasi anaweza kuviharibu au vinaweza kumletea madhara na mtoe eneo hilo.
Tusiadhibu watoto wetu wa umri wowote kwa kuwapiga au kuwachapa viboko, mtoto hawezi kuhusisha viboko na kosa alilotenda zaidi ya kuhisi tu maumivu ya fimbo.
Watoto wetu wanajifunza kutokana na yale tunayoyafanya kama wazazi, ni jukumu la mzazi kujaribu kuwa mfano wa kuigwa. Watoto ambao wamezoea kuona mama na baba daima ndani ni ugomvi, kupigana na matusi, watoto hao hawana amani na mara nyingi huishia kuiga tabia mbaya kutoka kwa wazazi hawa.

Miaka 3 hadi 5

Mtoto wa umri huu anaanza kujifunza na kuelewa mema na mabaya kutokana na matendo yake. Kuanzia umri huu anza kumfundisha mtoto sheria na taratibu za familia yako. Mfano kumsalimia baba na mama kila anapoamka asubuhi au kusema asante baada ya chakula au anapowewa kitu, kusalimia watu wanaomzidi umri nk.
Unapowapa watoto wa umri huu onyo au karipio waeleze kwanini kosa alilofanya ni kosa au kwanini alivyofanya si sahihi. Mfano mtoto amechora ukuta kwa rangi, mwambie rangi za kuchorea ni kwa ajili ya karatasi si kwa ajili ya ukuta na mwambie ukichora ukuta unaharibu mwonekano mzuri wa ukuta, hivyo asirudie.
Wakati unawajengea watoto ufahamu wa kipi ni kibaya ambacho wakifanya wataadhibiwa, ni vyema pia uwajengee nidhamu ya kuelewa kuwa ni mambo gani ambayo wakiyafanya vizuri watapata zawadi au wewe kama mzazi unayafurahia. Mfano, wazoeshe watoto umuhimu wa kufanya vizuri darasani. Waambie umuhimu wa kusoma, wajengee hamu ya kutaka kufika Chuo Kikuu nk na uwaeleze faida zake.
Watoto wa umri huu wanapokosa unaweza kuwapa adhabu kama vile kumtenganisha na vitu fulani fulani ili  kumjengea mtoto wa umri huu tabia nzuri. Mtenganisshe kwa muda ni vitu kama vile, kumzuia mtoto kungalia TV, kusikiliza redio, kucheza na wenzake kwa muda fulani nk.

2 comments:

  1. tumekupata mama familia,asante kwa mafundisho haya,

    ReplyDelete
    Replies
    1. Ahsante Neema karibu sana ujiskie upo huru na blog hii kuuliza au kutoa mada yoyote inayohusu familia na malezi ya watoto ili tusaidiane katika kulea watoto wetu vizuri.

      Delete